Music

Friday, April 11, 2014

NINAPOKUMBUKA MIAKA KADHAA YA KUZALIWA.....

Maalumu kwa mama yangu.
Ilikuwa tarehe 12th April 198…, saa mbili usiku jijini Arusha, ilikuwa siku ambayo familia ya Mesaya Simanga Masakoi na Tiinoi Mashon Kivuyo (Mr & Mrs Mesaya) walipotunukiwa na Mungu zawadi ya mtoto wa kiume. Najaribu kuvuta hisia zangu juu ya furaha waliokuwa nao vijana hawa wa enzi zile kwa kufanikiwa kumpata mtoto mwenye afya njema na ambaye alipofinywa kwenye kisigino cha mguu wake alilia mara tatu kuonyesha kwamba ni mwanaume rijali.

Mtoto huyu siku ya leo anatimiza zaidi ya miongo miwili na nusu tangu alipozaliwa. Ni kipindi kirefu sana kwa maisha ya mwanadamu wa siku hizi, lakini shukrani za pekee na za dhati zimwendee mwenyezi Mungu ambaye ameendelea kuwa mlinzi wake na msaidizi wake kwa magumu mengi ambayo amepata kupitia ama anapitia kwenye maisha yake ya kila siku.
Baada ya kutoa utangulizi huo sasa niende moja kwa moja kwenye kiini cha rai yangu hii ya leo ambayo nimeipa jina la “maalumu kwa mama yangu”. Leo ninapoazimisha siku hii ya kuzaliwa, nimependa nitumie muda wangu kuandika rai hii ya kumshukuru mama yangu kwa malezi bora na mema aliyonipatia hadi leo hii na mimi nimekuwa mtu kwenye kundi la watu.
Mama yangu mpendwa, najua waweza usipate bahati ya kusoma ujumbe huu moja kwa moja kutokana na kutokuwa na access na mitandao hii ya kijamii. Ila niweke tumaini kwamba ujumbe huu lazima utakufikia popote pale ulipo ama kupitia kwangu (mwanao), mtoto wangu (mjukuu wako), mchumba wangu, wadogo zangu, ndugu na jamaa zangu, marafiki zangu ama hata kupitia kwa walimwenguni wengine ambao wataona kuna haja ya ujumbe huu kutoka kwa uzao wako wa kwanza wa tumbo lako kukufikia.
Mama yangu mpendwa, hata kama ikatokea nikaitwa na mwenyezi Mungu kwa muda wowote, neno langu hili litakupa faraja na litaendelea kudumu milele na milele, vizazi na vizazi na hata jamii kwa jamii kwani hata maandiko yanasema na vile vile wahenga walipata kunena kwamba “mambo yote yatapita lakini neno litasimama”
Mama yangu mpendwa, nilipochukua jukumu la kuandika rai hii, nilipata shida sana kumalizia maneno kutoka aya moja kwenda aya nyingine kutokana na kububujikwa na machozi ya furaha na upendo wa dhati ulionao kwangu mwanao. Kila ninapomalizia mstari naona kama vile bado sijakidhi haja ya moyo wangu kueleza jinsi moyo wangu ulivyo na furaha kutokana na wewe kuwa mama yangu. Hakika hakuna kama wewe mama yangu.
Mama yangu mpendwa, ni miezi tisa (9) nimekaa ndani ya tumbo lako nikila na kujisadia kwenye tumbo lako, nikivuta na kupumua pumzi kwa msaada wa tumbo lako, nikicheza na kufurai ndani ya tumbo lako, nikirusha mikono na miguu ndani ya tumbo lako na…….dah, nakupenda sana mama.
Mama yangu mpendwa, nimeishi kwa kutegemea damu yako yaani ziwa lako kwa zaidi ya miaka miwili (2). Ukiwa na furaha, ukiwa na huzuni, ukiwa umechoka, ukiwa na haraka,, ukiwa na safari, na hata ukiwa na msiba, hata siku moja hukuninyima wala hukusita kunipa ziwa lako mama yangu pale nilipolihitaji.
Mama yangu mpendwa, kwa zaidi ya miaka 15 nimeishi na wewe, ukinielekeza yapi ya kuyafanya na yapi ya kutofanya kwenye jamii. Ukinielekeza tabia njema na nidhamu bora kama silaha itakayonisaidia niishi na ndugu, jamaa na jamii kwa ujumla.
Mama yangu mpendwa, hadi leo hii umekuwa kiongozi na mwalimu mzuri sana kwangu na kila nikaapo na wewe nahisi nimekaa kwenye kitovu cha elimu. Neno lako moja kwangu laweza kuwa na nguvu zaidi ya maneno elfu moja niliyowahi kusikia hapa duniani. Nasaha zako kwangu ni zaidi ya elimu niliyoipata shuleni.
Mama yangu mpendwa, sioni chochote chenye kuweza kuonyesha kiasi cha furaha na upendo nilionao kwako, ijapokuwa moyo wangu peke yake ndio unaojua na kulitambua hili. Laiti kama moyo ungekua na kioo ili uweze kuona ni jinsi gani jina lako na hadhi yako ilivyozungushiwa alama ya kopa na kuchukua sehemu kubwa sana kwenye moyo wangu, ungalithibitisha hili nisemalo. Lakini kwa kuwa siku hizi unaamini viungo vya mwili wako haviwezi kufikiri ama kutenda kinyume na matakwa yako, basi nami kama sehemu ama kiungo cha mwili wako niamini kwa haya niyasemayo.
Mama yangu mpendwa, sioni zawadi ya kukupa ambayo inaweza ikawakilisha ama ikatoa ufafanuzi wa kina juu ya upendo nilionao kwako. Zawadi pekee ni kutoa maisha yangu yote kukupenda kwa dhati. Naimani kwamba kwa maneno yangu haya ambayo yanatoka kwenye kiini cha moyo wangu, hata Mungu baba ataniongezea umri wa kuishi ukichukulia ya kwamba alitanabaisha kwenye amri zake kwamba “mpende baba yako na mama yako ili siku zako zipate kuwa nyingi katika nchi upewayo na Bwana Mungu wako”
Mama yangu mpendwa, nisikuchoshe sana kwa siku ya leo kwa kuandika rai ndefu sana, ila ujumbe huu ukufikie kwamba siku yangu hii ya kuzaliwa nimetoa maalumu kwako kama sehemu ya upendo wangu wa dahti nilionao kwako. Salamu na pongezi zote kutoka kwa ndugu, jamaa na marafiki zangu na wengine wote duniani za kunitakia kheri kwa siku hii zifanyike kuwa maombi ya kukuombea na kukutakia maisha mema, marefu na yenye amani na furaha hapa duniani na hata milele na milele.
Nakupenda sana mama, nakupenda sana mama, nakupenda sana mama, nakupenda sana mama, nakupenda sana mama, nakupenda sana mama, nakupenda sana mama……….

Nimeandaa na kuandika mimi mwanao mpendwa na uzao wako wa kwanza, Ismail Mesaya

1 comments:

  1. Makala naipenda kuliko makala zote nilizowahi kuandika

    ReplyDelete