Music

Sunday, April 6, 2014

Fukununu, makala muhimu sana kwenu wana-UDSM

CHUO KIKUU KIMEGEUKA CHOO KIKUU
Yapata miaka zaidi ya miaka miwili (2) toka makala hii iliyoshika kasi na kupendeza machoni mwa wasomi wa CHUO KIKUU ilipopotea kwenye mbao za matangazo za Cafteria na Getini Mabibo Hostel. Kwa wale waliokuwa sehemu ya umajimui huu wa UDSM, makala ya mwisho ilitoka tarehe 17th December 2011 ikiwa na kichwa cha habari kilichonakshiwa kwa maneno ya MCHAWI HUYU HAPA.

Makala ile iliyovuta hisia za walio wengi hasa ukizingatia hali halisi ya chuo kwa kipindi kile baada ya chuo kuwafukuza na kuwasimamisha masomo baadhi ya wanafunzi ambao utawala wa chuo waliwaita vinara wa migomo na maandamano.
Sina lengo la kuwakumbusha machungu hayo yaliyowakumba kaka zenu wala kuziamsha hisia zenu juu ya unyama na ukatili uliyofanywa na utawala wa chuo kikuu kwa shinikizo kutoka posta. Vile vile sina lengo la kuomba hisani kwenu kufanya “revenge” kwa hili lililotendwa na utawala wa Prof. R. Mkandala kwa moyo mweusi na uso uliokunjamana.
Baada ya tarehe ya mwisho ya makala hii kupotea kwenye mbao za matangazo, ilinilazimu kutafuta njia mbadala za kuendelea kufikisha makala ile machoni kwa wadau ambao walionekana kuongezeka kila kuitwapo leo. Niliona ni vyema nikitumia mitandao ya kijamii kuwafikia wasomaji wangu lakini pia kulikuwa na kikwazo kwani ningeweza kuwafikia wale walio marafiki kwangu pekee. Ndivyo nilivyoona ni vyema nikiwa na blog ambayo kazi yake ni kutawanya elimu ya fukununu kwa watu wote. Blogu hii ambayo nayo imeanza kupata umaarufu kwa makala zenye elimu kwa umma zinazochapishwa humo, inapatikana kwa http:fukununu.blogspot.com.
Nadhani kwa utangulizi huo kila mmoja wetu angalau kinaga ubaga ameshatambua wapi FUKUNUNU lilipotoka na nini hasa dhima yake. Nisipoteze kurusa nyingi kuendelea kutoa ulumbi juu ya makala hii, niende moja kwa moja kwenye mada kuu ya siku ya leo yenye jina la CHUO KIKUU KIMEGEUKA CHOO KIKUU.
Chuo kikuu kama walivyokisha tanabaisha walionitangulia ni kitivo cha ujuzi na maarifa. Chuo kikuu pia ni jukwaa la majadiliano na malumbano ya mawazo ili kuzaa mawazo kuntu kwa ajili ya mstakabali wa taifa letu na jamii zetu.
Mwalimu Nyerere aliwahi kusema; “A university must be a scholarly pitch where new thoughts are born”…… Kwame Nkuruma alinena kuwa “A university is a think tank”…… Sokoine aliwahi kukosoa juu ya wajibu wa wasomi waliopo vyuo vikuu kwa kusema, “maendeleo ya nchi yanafikiwa kwa kuwepo kwa midahalo na mijadala miongoni kwa wananchi juu ya namna gani tunaweza kufikia maendeleo hayo tunayoyataka, na kazi kubwa ya wasomi ni kuratibu na kuongoza majadilianao hayo”
Nukuu hizi zinaweza kusukuma mawazo yetu ili tufikiri zaidi nini maana ya chuo kikuu.
Chuo kikuu hiki kimekuwa ni chimbuko la mawazo kuntu ambayo yamewezesha nchi nyingi za afrika kupata uhuru na pia kitovu cha maendeleo kwa nchi yetu hasa enzi za utawala wa Mwalimu. Mapambano ya kudai uhuru wa Mozambique mwaka 1975, iliyokuwa South Rhodesia mwaka 1980 na hata harakati za kupinga ubaguzi wa rangi nchini Afrika ya kusini, yalifanywa na wanaharakati waliokuwa sehemu ya umajimui wa chuo kikuu hiki wakitumia eneo liligeuzwa kwa sasa na utawala wa UDSM kuwa eneo la kutunzia majani ya mifugo. Eneo hili si linguine bali ni lile lililowekewa uzio na utawala wa UDSM kana kwamba kuna biashara haramu iliyokuwa ikifanyika pale na kwa chini wamegeuza soko kwa kuwakodishia wafanyabiashara ili tukuharamisha matumizi ya awali ya eneo lile.
Eneo hili maarufu kwa wanasiasa na viongozi mbalimbali wa bara la afrika waliopata kusoma hapa chuo kikuu cha Dar es salaam, kwasasa ni eneo ambalo ni haramu kutolea mawazo na kwa yeyote atakayefanya hivyo atakuwa amejitafutia barua ya kufukuzwa chuo mara moja na moja kwa moja. Kwa wale walioko mwaka wa pili na wa kwanza wa masomo wangetamani kulifahamu eneo hili ambalo lilipata kutumiwa na watu kama, John Garang’, Joseph Kabila, Yoweri Museveni, Zakiah Meghji, Samwel Sita, Issa Shivji, Jakaya Kikwete, John Mnyika, Julius Mtatiro, James Mbatia, Yonas Laiser, Alphonce Lusako, Mwambapa Elius, Ambros Evarest, Oduor oduang’, Ismail Mesaya, Zito Kabwe, na wengine wengi katika kutetea haki na maslahi ya makundi mbalimbali katika jamii zao na nchi zao. Kwa jina maarufu eneo hili linajulikana kwa jina la REV. SQUARE ikiwa na maana ya REVOLUTION SQUARE.
Katika kuwaziba midomo na kugeuza chuo kikuu kuwa sawa na shule ya msingi, watawala wameamua kulifunga eneo hili na kuharamisha mijadala na midahalo yote yatakayofanywa na wanafunzi wake. Kwa kufanya hivi tunatengeza taifa lenye watu wasio na uwezo wa kuhoji, kulinda na kutete haki na maslahi yao katika Nyanja mbalimbali.
Chuo kikuu kiwe ni sehemu ya kuwandaa vijana kurithi nafasi mbalimbali na kulitumikia taifa lao. Chuo kikuu kitumike kutengeneza taifa lenye watu wenye utashi wa kuhoji na kunyooshea kidole pale panapoonekana kutendwa kinyume na taratibu. Chuo kikuu kitumike kuwaandaa wanachi wenye utashi na udhubutu wa kuwawajibisha wale waliopewa dhamana kuwatumikia katika sekta mbalimbali. Chuo kikuu kiwatengeneze watumishi na wafanyakazi wenye kukubali kushauriwa na kukosolewa. Chuo kikuu kiwe chachu na kitovu kikuu cha kusukuma maendeleo  ya nchi yetu.
Chuo kikuu kisiwe sehemu ya kutengeneza jamvi la wasomi wa wa makaratasi wasio na uwezo wa kuhoji, kutetea na kufanya mambo mengine kuntu kwenye jamii zaidi ya kile kilichopo kwenye makaratasi.

Nawaomba wale wahusika walifikiri hili suala kwa kina kwa maslahi ya nchi yetu na jamii zetu na pia kuwatengeneza watumishi na wafanyakazi wenye manufaa chanya kwa taifa.

Imeandaliwa na kuandikwa:
Jina: Mesaya Ismail
Cont: +255 756 688 090

0 comments:

Post a Comment