Music

Tuesday, December 9, 2014

JE, NI HALALI KUTANGAZA NA KUSHEREKEA TAREHE 9/12 KAMA SIKU YA UHURU WA TANZANIA???


JE, NI HALALI KUTANGAZA NA KUSHEREKEA TAREHE 9/12 KAMA SIKU YA UHURU WA TANZANIA???
Ilikuwa mwaka 1954, Julius K. Nyerere mwalimu wa shule ya sekondari na mmojawapo kati ya watanganyika wawili waliokuwa na elimu ya chuo kikuu walipounda chama cha TANU, ambacho kilichochea na kusukuma harakati za kudai uhuru na hatimaye tarehe 9/12/1961 nchi ya Tanganyika ilipata uhuru na Mwl. J.K.Nyerere akawa waziri mkuu chini ya katiba mpya.
Mwaka mmoja baadaye yaani 9/12/1962, Tanganyika ilikuwa Jamhuri na Mwl. J.K Nyerere akawa rais wa kwanza.

Mwaka 1964 April 26, Mwl. J.K.Nyerere (Rais wa Jamhuri ya Tanganyika) na Sheikh Abeid Aman Karume (Rais wa serikali ya watu wa Zanzibar) waliridhia na kuazimia kuunganisha nchi zao yaani Tanganyika na Zanzibar, na kuunda NCHI MPYA ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania.
Muungano huu wa nchi hizi mbili ulififisha na kudhoofisha uwepo wa nchi washirika yaani Tanganyika na Zanzibar ili kuipa nafasi nchi mpya ya Tanzania kujitengenezea mipaka na historia yake. Kwa tafasiri nyepesi tunaweza kusema historia ya Tanganyika ilibaki kama historia ya nchi mshirika yaani Tanganyika na haikurithiwa ama kukasimiwa kuwa historia ya TANZANIA. Vivyo hivyo kwa upande wa Zanzibar. Hii ina maana kwamba historia ya nchi hii mpya ya Tanzania ilipaswa kuanza kutengenezwa siku na tarehe ilipozaliwa yaani 26/04/1964. Kutengenezwa kwa historia hii ya Tanzania haina maana ya kufuta historia za nchi washirika, kama vile ujio wa wakoloni, harakati za mapambano ya uhuru na historia yote kabla ya muungano kama utamaduni, utawala, mila na desturi.
Hoja yangu hiyo inatokana na ukweli kwamba muungano wetu haukuasisiwa ili kufuta historia za nchi washirika. Ili kutoa nguvu kwa nchi mpya ya Tanzania kujitengenezea historia yake yapaswa shughuli zote za kihistoria za nchi washirika kusimamiwa na kuasisiwa na nchi husika yaani nchi mshirika. Kwa lugha nyepesi tunaweza kusema masuala kama vile maadhimisho ya siku ya uhuru wa Tanganyika, yapaswa kufanywa na kusimamiwa na nchi mshirika yaani Tanganyika na sio Tanzania. Vivyo hivyo kwa masuala ya mapinduzi ya Zanzibar yanapaswa kufanywa na kusimamiwa na serikali ya Zanzibar (kama ilivyo sasa). Suala pekee ambalo linapaswa kufanywa chini ya mwamvuli wa Tanzania (yaani muungano) ni maadhimisho ya siku ya muungano tu. Kwa kufanya hivi tutakuwa tumetoa nafasi kwa nchi washirika kuendelea kuenzi na kukumbuka historia yao, na vile vile tutakuwa tumetoa wigo mpana kwa nchi mpya ya Tanzania kujitengenezea historia yake.
Hali ilivyo kwasasa
Kwasasa tunaona kwamba masuala yote yanayohusu historia ya Tanganyika yamekasimishwa kwa nchi mpya ya Tanzania na yale yanayohusu Zanzibar yamebaki kwa wazanzibar.              Hii inadhihirishwa pale siku ya tarehe 9/12/1961 siku ambayo nchi ya Tanganyika ilipata uhuru, inapogeuzwa na kufanywa ni siku ya uhuru wa Tanzania. Maswali ya msingi ya kujiuliza ni:
i)                    Je, Nchi ya Tanzania iliwahi kutawaliwa? Je ilitawaliwa na koloni gani?
ii)                  Je, Nchi ya Tanzania iliyozaliwa 1964 kwa muungano wa nchi mbili huru yaani Tanganyika na Zanzibar, ilipata uhuru lini? Chini ya chama gani? Kutoka kwa ukoloni wa nchi gani? Muasisi wa harakati hizo alikuwa nani?
iii)                Je, Ni halali kufuta historia ya Tanganyika na kuikasimisha kwa nchi mpya ya Tanzania?
iv)                Je, Hatutakuwa tunadanganya na kupotosha vizazi vijavyo kwa kuwarizisha kwamba Tanzania ilipata uhuru desemba 9 1961?
v)                  Je, Ni kwanini linashindikana kwa hili la historia ya Tanzania kuandikwa kama ilivyo pasipo kuchanganya na historia ya Tanganyika, lakini limewezekana kwa historia ya TANU kutenganishwa na kuandikwa tofauti na historia ya CCM ambayo nayo imetokana na muungano wa vyama vya ASP na TANU? Yaani leo hii hatuwezi kujinasibu kwamba CCM ilizaliwa rasmi tarehe 7/7/1954 siku ambayo TANU ilizaliwa, kama tunavyofanya kwa kusema Tanzania ilipata uhuru 1961 siku ambayo Tanganyika ndiyo ilipata uhuru.
vi)                Je, Ni nani wa kutunusuru kutoka kwenye upotoshaji huu kama wasomi, wanasiasa na makundi mbalimbali ya kijamii yamejikita kuhalalisha uongo huu bila kukosoa?
Hatuwezi kukwepa kukabiliana na masawali haya kama kweli tuna nia ya dhati ya kulinda na kuenzi historia za nchi washirika wa Muungano, na vile vile kukuza na kuendeleza nchi hii mpya ya Tanzania ambayo ina miaka 50 kamili kwenye uso wa dunia toka ilipozaliwa.
Kwa kuendelea kutenda kama tunavyofanya kwa sasa kwa kuruhusu kwa makusudi kufutika kwa historia ya nchi ya Tanganyika, mambo kadhaa nayaona:
a)      Kuwa muungano wa Tanganyika na Zanzibar haukuwa na lengo la kuunganisha nchi mbili huru na zenye historia kamili, bali ulikuwa ni ujanja wa nchi moja kubadili jina na kuitawala nchi nyingine. Yaani nchi ya Tanganyika ilibadili jina na kuitwa Jamhuri ya Tanzania na kutawala nchi ya Zanzibar. Hii inadhihirishwa pale tunapoona masuala yote ya kihistoria, kiutawala, kikatiba, kisiasa, mila na tamaduni za Tanganyika zikikasimiwa na kurithiwa na nchi mpya TANZANIA
b)      Kuwa kitendo cha nchi ya Tanzania kutumia rasilimali fedha ambazo zimekusanywa kutoka kwenye vyanzo vya mapato ambazo ni za pande zote za muungano, vyombo vya usalama, utawala wa nchi ya Tanzania (rais) kuandaa na kutekeleza shughuli zihusuyo historia ya nchi  ya Tanganyika, ni unyonyaji na ufisadi wa rasilimali za Zanzibar kwani siku ya maadhimisho ya mapinduzi ya Zanzibar hufanywa na serikali ya watu wa Zanzibar na sio serikali ya muungano.
c)      Kuwa muungano umelenga kwa makusudi kufuta nchi ya Tanganyika na historia yake katika uso wa dunia. Hii inadhibitishwa pale tunapoona masuala yote ya kihistoria yanayohusu Tanganyika yakirizishwa kwa nchi ya Tanzania. Vile vile kitendo cha kuondoa uhalali wa nchi ya Tanganyika kikatiba na kufanya katiba ya Tanzania kuwa ndio katiba ya Tanganyika ni kuhalalisha kile nilichokiita Tanganyika kubadili jina kwa lengo la kutawala Zanzibar.
Hitimisho
Ili tusihukumiwe na historia na tuwatendee haki vizazi vijavyo hatuna budi kutenganisha masuala ya Tanganyika na yale yanayohusu Tanzania. Kwa mfano masuala ya maadhimisho ya siku ya uhuru wa Tanganyika, yaani tarehe 9/12 yanapaswa kusimamiwa na utawala wa nchi ya Tanganyika ambapo kwa katiba ya sasa yanapaswa kusimamiwa na Waziri mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwani ndiye msimamizi wa shughuli za kiutawala zihusuyo Tanganyika.
Vile vile hatuna budi kubadili katiba yetu ili kutoa mwanya kwa nchi washirika wa muungano kuenzi historia zao na nchi mpya ya Tanzania kujitengenezea historia yake.
Pia tubadili maandiko yetu yanayotumiwa kama zana za kufundishia mashuleni na tuweke wazi ukweli kuwa Tanzania haijawahi kutawaliwa bali imezaliwa rasmi 26/04/1964 kwa muungano wa nchi mbili huru zenye historia zao. Hii itasaidia kuondoa fikara kwamba tarehe 9/12/1961 ni siku ya uhuru wa Tanzania. Vile vile hii itasaidia kuenziwa kwa historia ya nchi hizi washirika na historia ya Tanzania (nchi mpya) kujengwa kwenye fikra za vijana na vizazi vijavyo.
Hongera Tanganyika kwa kufikisha miaka 53 ya uhuru. Utulivu wako uendelee kudumu daima kwa vizazi na vizazi.
@Ole Mesaya
Cont: +255 756 688 090

0 comments:

Post a Comment