Music

Wednesday, March 26, 2014

Mwanafunzi fanya hivi upate kufaulu....P.II

MWANAFUNZI FANYA HIVI UPATE KUFAULU MITIHANI YAKO YA TAIFA
Awali ya yote niwasalimu na kama ilivyo ada kwa tamaduni zetu za kiafrika baada ya salamu kifuatacho ni kujualiana hali ya familia na utokako. Vivyo hivyo na mimi niwe na tumaini moyoni kwamba wewe msomaji wa makala hii u mzima na bukheri wa afya pamoja na familia yako.
Leo nimelenga kutoa darasa kwa wanafunzi wa shule za sekondari juu ya nini cha kufanya ili aweze kuhesabiwa kwenye lile kundi la wanafunzi wenye daraja la kwanza ama la pili na/ama kuondoka kwenye lile ombwe la wanafunzi wenye daraja la nne na daraja sifuri.
Mada hii inalenga kumtanabaisha mwanafunzi wa sekondari kuanzia ngazi za awali kabisa juu ya namna gani ajiweke ama afanye nini ili hatimaye mwishoni apate matokeo mazuri. Pia kama wale walio na mitihani ya taifa hasa kidato cha nne na sita wanaweza kutumia kanuni hizi wakati wakijiandaa na mitihani yao ya taifa.
Nisipoteze kurasa nyingi katika kujadili utangulizi wa mada, sasa nilenge moja kwa moja kwenye kiini cha mada. Kama mada inavyojitutumua kwa kichwa cha somo kilichonakishiwa kwa maneno “Mwanafunzi fanya hivi upate kufaulu mitihani yako ya taifa” nami nitoe ulumbi wangu kwamba nalikua namaanisha nini kwa somo hili.
Somo hili linalenga kutoa njia ama kanuni anuai zitakazomsaidia mwanafunzi kufanya vizuri katika mitihani yake kama atazifuata na kusizingatia. Kanuni hizi nimezitengeneza mwenyewe kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa elimu wakiwemo wanafunzi, walimu, wazazi, viongozi na makundi mengine mbalimbali kwenye jamii ambayo yana mapenzi ya dhati kwenye sekta hii ya elimu.
Kanuni (principles) za kufaulu
1.      Fahamu sababu yako ya kusoma (Tambua ni kwanini unasoma) (Reasons for being at school)
Wanafunzi walio wengi hata baadhi ya wazazi (hasa wa jamii ya wafugaji, wakulima, wavuvi na warinaji) hawatambui ni kwanini wanasoma/wanawaelimisha watoto wao.
Mtoto anapozaliwa jamii inashangilia na kupiga vigelegele kwa kumpata mtoto ila ni wachache sana kwenye jamii wanaokuwa tayari wamekwisha kuandaa mazingira endelevu kwa mtoto wao. Mazingira endelevu ni pamoja na kumwandalia mototo mpango mkakati wa muda mfupi na muda mrefu yaani wa kuanzia miaka 0-5, 5-10, 10-15, 15-25. Ili kumwezesha mtoto kuweza kukabiliana na hali halisi ya mazingira ya dunia ya sasa na kutomtengezea maisha magumu, wazazi hawana budi kuwatengenezea malengo watoto wao kuanzia ngazi ya awali kabisa, yaani pale wanapokuwa ujawazito. Hii itawasaidia kuwa na familia bora ambayo wanaweza kuimudu na kuihudumia kuanzia soksi hadi kofia.
Kwa upande wa mtoto ni lazima atambua ni kwanini wazazi wake wakampeleka shule, ni kwanini wazazi wake wanatumia gharama nyingi kumsomesha, ni kwanini wazazi wake wanatumia muda mwingi kuhangaika na elimu yake. Tathimini hii yapaswa kufanywa na mwanafunzi kwa kutambua umuhimu wa elimu kwake.
a)      Elimu ni silaha itakayomsaidia mwanadamu kukabiliana na mazingira na changamoto za kila siku za maisha.
b)      Elimu ni jamvi litakalomsaidia kijana kupokea na kurithi mila, tamaduni na desturi za taifa lake. Kwa kusema mila, desturi na tamaduni za taifa namaanisha tunu na rasilimali za taifa.
c)      Elimu ni maji yatumikayo kunyeshea mipango na miradi mbalimbali ya mwanadamu na taifa lake kwa ujumla.
d)     Elimu ni chombo kitakachomsaidia mwanadamu kutumia rasilimali na tunu zilizopo kwa manufaa chanya kwa jamaa na jamii yake
Hizi ni baadhi tu ya umuhimu wa elimu kwa jamii. Hivyo kama mwanafunzi anapaswa atambua anasoma ili apate elimu itakayomsaidia kukabiliana na yaliyotanjwa hapo juu.
2.      Fahamu/Tambua thamani yako kama mwanafunzi (Your value as a student)
Katika jamii yetu ya kitanzania na hata dunia nzima, mwanafunzi ni cheo ambacho kinaheshimiwa sana na makundi mbalimbali ya watu katika jamii. Heshima hii inatolewa na jamii kwasababu wanatambua kwamba “mwanafunzi” ni mtu anayeandalia kupokea na kurithi tunu na rasilimali za taifa kwa maendeleo ya taifa husika. Kwa kupitia wanafunzi ndipo tutakapo wapata viongozi, madakitari, walimu, wanasheria, wahasibu, wahandisi, wakufunzi na wataalamu mbalimbali. Vivyo basi ni lazima mtu huyu apewe dhamani ili baadaye tumpate mtu sahihi tunayemtaka kumkabithi tunu na rasilimali za taifa letu.
Kwa mfano tu mrahisi, leo hii wanafunzi (wakiwa wamevalia sare za shule) wakivuka barabara katika miji yetu magari husimama ili kuwapisha wanafunzi hao wavuke. Vile vile siku hizi tunaona pia jamii imekuwa ikichukua jukumu la kuwavusha wanafunzi barabara pale panapo onekana kuna magari yanayoenda kwa kasi. Si hilo tu, jamii imekuwa ikichukua hatua mathubuti kwa yeyote atakayeonekana akifanya jambo ambalo linahatarisha maendeleo ya mwanafunzi shuleni. Mfano ukionekana unaingia gest na mwanafunzi jamii itakuchukulia hatua haraka, vile vile ukionekana unawauzia wanafunzi madawa ya kulevya pia jamii haitosita kukuchukulia hatua. Hata serikali inalitambua hili na kuwadhamini wanafunzi ndio maana wanafunzi wana gharama zao za usafiri tofauti na watu wengine.
Vivyo hivyo kwa mwanafunzi ni lazima atambue heshima hii anayopewa na jamii na ajaribu nayeye kuheshimu cheo hiki kwani kwa kufanya hivyo atakuwa amewaheshimu jamaa wa jamii ile na vile vile ameheshimu dhamana ile aliyopewa. Mwanafunzi ni lazima afananie na cheo chake na heshima ile anayopewa. Mwanafunzi avae mavazi yanayoendana na cheo na thamani yake. Mwanafunzi awe ni mfano wa kuigwa kwenye familia na jamii yake kwa kufanya vile ambavyo vitalinda na kutunza cheo na heshima yake.
3.      Kuwa na malengo (Your targeted objectives)
Mwanadamu yeyote anapoanza kufanya jambo lolote, huwa na malengo si ya kumaliza jambo husika bali ni kufanikisha lengo la kufanya jambo hilo. Kwa yeyote anayefanya hivi mara nyingi huwa na mipango mikakati na sera (strategies and policies) za kumwezesha kufikia malengo tajwa (Targeted objectives) kwenye jambo hilo.
Kwa upande wa wazazi, hapana budi kuwa na malengo na kupanga njia na mipango mikakati za kumwezesha mtoto wao kufikia malengo hayo. Kwa mfano waweza kuwa na lengo la kuhakikisha mwisho wa siku mtoto anapata alama daraja la kwanza katika mitihani yake ya mwisho ya kidato cha nne na vile vile kupata daraja la kwanza katika mitihani ya mwisho ya kuhitimu kidato cha sita. Kwa kuwa na lengo hili itakulazimu wewe kama mzazi kumtafutia kijana wako huyo vitabu vya kutosha, kumlipia masomo ya ziada, kuwa karibu na walimu na kufuatilia maendeleo yake kwa ukaribu mkubwa na kila wakati. Vile vile mzazi muekee kijana huyo malengo ya muda mfupi ambayo yatamsaidia kufikia lengo husika katika mitihani ya mwisho kwani kama wasemavyo wahenga, mafanikio ya kesho yanahitaji maandalizi ya leo.
Kwa upande wa mwanafunzi, pale anapopevuka kiakili ama pale anapofanikiwa kujiunga na masomo ya sekondari ni lazima awe na malengo kama nilivyoainisha hapo juu. Vivyo hivyo kwa mwanafunzi huyo pia, aweke mipango mikakati ya muda mfupi yatakayo mwezesha kufikia malengo yake.
Division one na two vyote vinawezekana kama pande zote zitaweka malengo ya kupata madaraja hayo kuanzia ngazi ya awali mtoto anapoanza shule ama hata anapojiunga na masomo ya sekondari
4.      Kuwa na imani (Be faithful)
Labda hili nianze kulizungumzia kwa kutoa mfano, “……..siku zote mtu unapoelekea nyumbani kwako/kwenu, unakuwa na tumaini kubwa zaidi hata ya 100% kwamba utafika nyumbani. Hapana hata siku moja ambayo umewahi kuwa na wasiwasi kuwa yawezekana pale unapoenda patasogea mbele kidogo ama karibu kidogo kukufuata. Wala hutawaza kwamba yawezekana mahala pale pakawa angani ama kujichimbia ardhini……..” Sasa kama wote tuanakua na imani hiyo basi hata kwenye masomo yetu tukiweka imani hiyo hakika tutafanikisha lengo husika. Niwakumbushe pia kwamba hapana hata siku moja unaweza kufikia lengo ukiwa umakaa ama kwa lugha nyingine umebweteka yaani pasipo kujishughulisha, hata huyo anayesafiri kwenda nyumbani kwake anakuwa na malengo kuwa atafika nyumbani kwake/kwao pale tu atakapochukua hatua kadhaa kuelekea kule, lakini akiwa na malengo hayo ilihali amekaa tutafananisha imani hiyo na ndoto za Abunuazi.
Kwa wale wanaoamini katika dini ya kikristo, kitabu takatifu cha Bibilia katika Waraka wa Mtume Paulo kwa Waebrania sura ya kumi na moja mlango ule wa kwanza hadi ule wa mwisho wa thelathini na mbili (Ebr.11:1-32) sura yote hiyo inazungumzia imani na baadhi ya shuhudu zenye kujenga imani (faithfulness) ya mtu. Sasa kwa kutumia maandiko hayo, nasi tunaweza kuwa na imani kwamba division one and two are within our scope and we can achieve, but don’t forget to struggle for it.
5.      Kuwa mshindani (Be competent)
Katika mashindano yoyote hata ya kufukuza kuku au ya kula andazi, kila mshiriki huwa anaingia pale akiwa na lengo la kwamba atashinda. “……….Before trial, all probabilities are equals to one……..” Hii inamaanisha kwamba kabla ya michuano yoyote kuanza kila mtu uwezekano wake wa kuibuka mshindi ni moja.
Tuje kwa upande wa elimu na masomo, ila nianzie kwa mzazi. Mzazi yeyote anayependa maendeleo ya mwanae hana budi kumtengenezea mtoto wake mazingira ya kuwa mshindani. Kwa mfano, unaweza ukampa mtoto ahadi ya kwamba kama atapata wastani wa alama kuanzia 61 na kuendelea utampeleka mbuga za wanyama. Mtoto huyo akifanikiwa kupata mtimizie ahadi hiyo. Na kama atashindwa kufikisha, usimkatishe tama, mpongeze kwa alama zile alizopata na mpe ahadi nyingine bora zaidi ambayo itamfanya aongeze bidii zaidi.
Kwa upande wa wanafunzi, unapokuwa darasani huna budi kujitengenezea alama ambazo unataka kuzipata kwa kila somo. Usiwe mzembe ukijiwekea alama za chini kwani utakua ni sawa na yule mwizi anayeiba mfuko wa kulia na kuweka mfuko wa kushoto. Panapotokea hujaweza kufikia malengo hayo, jiulize kwanini mwenzako mnayesoma naye amefikisha alama hizo. Ikiwezekana tengeneza urafiki naye ili akupe mbinu anazotumia kupata alama za juu.
6.      Fanya kusoma ni sehemu ya maisha (Make reading a part and parcel of your daily life and routine)
Wanafunzi hujisifu kwa kufanikiwa kukesha wakiwa na vitabu ama hujinasibu kwa kufanikiwa kusoma twisheni ya masomo yote. Jambo la msingi la kufanya si kusoma kwa kukesha, ama kusoma twisheni ya masomo yote, kwa maana njaa haimalizwi kwa kula sana bali pale utakapohisi. Mwanafunzi anatakiwa atambua kwamba cheo na hadhi yake ni “uanafunzi” hivyo popote pale atakapojisikia kufanya shughuli yake iliyokuu ya kusoma na asome. Pamoja na hayo kila mwanafunzi na awe na ratiba yake ambayo itamfanya angalau kwa siku nzima ya masaa 24 atumie masaa 8 kila siku kusoma. Masaa haya ni tofauti na muda ambao mwalimu anakuwa darasani. Kwa kutumia ratiba hiyo mwanafunzi atalazima kufuata na ikitokea ameikosea ratiba itabidi atafute muda wa ziada ya kutilimiliza ratiba hiyo (find the alternative ways to supplement the lost time). Vile vile pamoja na kuwa na ratiba hiyo, mwanafunzi hana budi kufanya kazi yake kuu yaani kusoma pale anapojisikia kufanya hivyo hata kama ni nje ya muda husika. Mfano, unapoweka ratiba kwamba kula ni saa nane mchana, ikitokea ukasikia njaa saa sita mchana hutaacha kula. Vivyo hivyo na kusoma pia.
Nihitimishe kwa kuwaasa pande zote na wadau wote wa elimu kwamba mustakabali na maendeleo ya elimu yetu ipo mikononi mwetu na si mikononi mwa mwalimu na mwanafunzi pekee. Tukumbuke ya kwamba hata mashine ili iweze kufanya kazi vizuri na kutoa output nzuri lazima kuwe na ukaribu na resources zote zinazohitajika, ikiwa ni pamoja na input sahihi, mwanadamu mwenye uzoefu, machine bora na nzima, umeme na vingine vinavyotakiwa kuendesha mashine.
Pia kwa upande wa wazazi tukumbuke kwamba mafanikio ya mtoto wako ni mafanikio yako. Kwa walimu msisahau kwamba mafanikio ya mwanafunzi ni tuzo na inaongeza credit kwenye taaluma yako. Na kwa mwanafunzi usisahau kwamba mafanikio yako ni heshima kwa wazazi, jamaa, jamii na taifa lako kwa ujumla.
Imeandaliwa na kuandikwa na,
Jina: Ismail Mesaya
Simu: +255 756 688 090
          +255 712 814 285


0 comments:

Post a Comment