Music

Saturday, February 3, 2018

WARAKA WANGU KWA WAZIRI WA ELIMU (JOYCE NDALICHAKO)

Asalaam Aleikumu watanzania wote wenye imani ya Kiislamu. Tumsifu Yesu Kristo kwa wale wenye imani ya Kikristo. Fuatana name kwenye makala yangu hii kwa Mama Joyce Ndalichako (Waziri wa Elimu)

Mama Ndalichako Shikamoo. Natumaini wewe ni mzima bukheri wa afya tele. Sisi huku Nadosoito hatujambo tuko na afya njema kimwili ila akili zetu ziko nzito kutokana na wale watoto wetu Naropil, Namelok na wale wa mzee Leshabar kushindwa kupata alama nzuri kwenye matokeo yao ya mitihani ya kidato cha nne.
Mama Ndalichako, hali hii imenifanya nami nichukue kalamu na karatasi niunde silabi kutoa maoni yangu juu ya suala hili kwani kadiri siku zinavyozidi kwenda mbele hali inazidi kuwa mbaya.
Mama Ndalichako, nitachanganua baadhi ya mambo yanayochangia mdororo huu wa elimu kwa kutumia kijiji changu cha Nadosoito kama eneo la tafiti.
Mama Ndalichako, jambo kuu lililochangia mdororo huu huku kwetu ni kubadilika kwa muundo na mfumo wa elimu. Mabadiliko haya hasa kwa upande wa shule ya msingi ndio umeleta matokeo haya kwa elimu ya sekondari.
Mama Ndalichako, awali wakati mimi na kaka yangu tunasoma, tulianza darasa la kwanza na la pili, Mwalimu Chacha alikuwa anatufundisha 3K (Kusoma, Kuandika na Kuhesabu). Si unamkumbuka yule mtoto wa Mzee Menyengera ambaye alikuwa hajui kusoma na kuandika alirudia darasa la kwanza mara mbili hadi alipojua kusoma na kuandika ndipo aliendelea na madarasa mengine??? Sasa hali hii ilikuwa inafanya watoto wanaochaguliwa kuendelea na kila darasa awe ana uwezo wa kukabili masomo ya darasa husika.
Mama Ndalichako, unakumbuka ule mtihani wa taifa wa darasa la nne 1999, lile darasa letu walifeli wanafunzi wangapi?? Unamkumbuka yule binti wa Mzee Leng’ojine ambaye alianza darasa la kwanza mwaka 1992 lakini alihitimu darasa la saba mwaka 2002? Nimekukumbusha scenario hizi mbili ukumbuke jinsi ule mtihani wa darasa la nne ulivyokuwa unatumika kuwachuja watoto na kuruhusa tu wale wenye uwezo kuendelea na darasa la tano.
Mama Ndalichako, sina shaka unakumbuka kipindi kile ukiwa Necta, wastani wa alama za ufaulu kwa mtihani wa darasa la saba. Nakumbuka Mwalimu Mondare alikuwa anatuasa na kutusisitiza sana kusoma ili tufanikiwe kupata alama zile ambazo kwa wavulana ilikuwa alama 93/150 na wasichana ilikuwa ni alama 90/150. Kipindi kile mtihani wa darasa la saba ulikuwa ni masomo matatu (Maarifa, Lugha na Hisabati). Kila somo lilikuwa na alama 50 hivyo kufanya masomo matatu kuwa na jumla ya alama 150.
Mama Ndalichako, unakumbuka kipindi hiko wale wanapata alama za juu zaidi walikuwa wanachaguliwa kujiunga na shule za sekondari za vipaji kama Ilboru, Mzumbe, Tabora boys, Msalato, Kibaha, Kilakala. Halaf wale ambao wamekosa nafasi kujiunga na shule za serikali (ambao wengi wao walikuwa ni wale wenye alama chini ya wastani wa kufaulu) ndio waliokuwa wanajiunga shule za binafsi. Hii ndio ilikuwa sababu kwa shule za serikali kufanya vizuri zaidi kuliko shule za binafsi hali ambayo iliwafanya wazazi wawe na imani sana kwenye shule za serikali kuliko za binafsi hivyo kuwahasisha watoto wao kusoma kwa bidii ili wachaguliwe kujiunga na shule za serikali.
Mama Ndalichako, nikurudishe tena kwenye kumbukumbuku zako za enzi zile, pamoja na alama za ufaulu kuwa juu zaidi kwa darasa la saba, bado kulikuwa na mtihani wa kidato cha pili ambao ulikuwa unawachuja wale wote wenye wastani wa alama chini ya 36 (D). Hii imenikumbusha wale vijana 24 wa darasa letu waliorudia kidato cha pili akiwepo yule kijana wa Mzee Lemutan.
Mama Ndalichako, mchujo huu wa kipindi kile ulikuwa na faida zifuatazo:
1} Ulikuwa unawahamasisha sana wanafunzi kusoma kwa bidii kuepuka aibu ya kurudia darasa
2} Ulikuwa unawaandaa wanafunzi kuwa watafutaji na wapambanaji katika masomo yao ili kukwepa aibu ya kurudia darasa
3} Ulikuwa unaongeza chachu ya ushindani kati ya mwanafunzi na mwanafunzi na kati ya shule na shule. Hii ilichangia sana kuongeza ufaulu na vipaji kwa watoto
4} Ulikuwa umejenga imani kubwa sana kwa wazazi na jamii kwa ujumla juu ya shule za serikali wakiamini kwamba wale wanaofaulu pekee ndio walipata nafasi ya kujiunga na shule za serikali
Mama Ndalichako, hatua ulizochukua hizi karibuni, kwa mtizamo wangu naona unaenda kujenga taifa lenye vijana wengi waliofika kidato cha nne wasio na elimu wala taaluma ya kidato cha nne. Hatua hizi utadidimiza zaidi imani ya jamii kwa shule za serikali lakini pia utafanya ufaulu uwe chini zaidi ya ulivyo sasa. Mama natumai unaelewa kwamba, ili kujenga taifa imara ni lazima tuwe na mfumo wa elimu ambao unawandaa vyema vijana kurithi tamaduni na desturi za taifa kutoka kizazi kimoja na kurithisha kizazi kingine. Hiyo ndio dhima kuu ya elimu ambayo ina lengo la kujenga na kuimarisha taifa kwa mustakabali wa vizazi vijavyo.
Mama Ndalichako, nashauri yafuatayo yafanyike kama kweli tuna nia ya kuboresha elimu yetu na kurudisha imani ya shule za serikali katika jamii. Pia utakuwa ni mfumo ambao unawandaa vijana wabunifu na watafiti ili waweze kuwa machampioni wa kulinda na kutumia rasilimali tulizonazo kwa maslahi ya jamii yetu na taifa kwa ujumla.
11)      Turejeshe mchujo kama ulivyokuwa awali. Yaani mwanafunzi pekee atakayeruhusiwa kuendelea na darasa la tatu ni yule tu anayejua 3K. Vivyo hivyo kwa darasa la nne na kidato cha pili kuwe na mitihani ya mchujo.
22)     Turejeshe alama zile za ufaulu wa mwanafunzi wa darasa la saba kwenda kidato cha kwanza kuwa ni wastani wa alama 31/50 kwa kila somo. Hapa nitatoa mchanganuo ninaopendekeza na faida zake:
a)      Shule za secondary zigawanywe katika makundi mawili. Moja, Shule za Sekondari zinazotoa elimu kama ilivyo sasa. Pili shule za elimu ya ufundi.
b)      Alama za ufaulu ziwe: 31/50-50/50 wananfunzi hawa watajiunga na elimu ya secondary. Elimu hii inawajenga sana wanafunzi katika usimamizi, uongozi wa rasilimali zetu. Alama zote chini ya 30/50 wanafunzi hao wagawanywe katika makundi kuendelea na elimu ya ufundi kutegemea ufanisi wa kila mmoja. Elimu ya ufundi ni kama Kilimo, Ufugaji, Uchimbaji madini, Uchongaji, Uselemala, Uwashi, Urinaji, Uvuvi nk.
c)      Wanafunzi wote watakaofaulu kwenye mifumo yote miwili yaani wa technical na nontechnical watakutana Chuo Kikuu kuchukua elimu ya juu zaidi kwenye taaluma yake. Utakuja kuona kwamba wale watakaofeli elimu ya sekondari watarudi kuendelea na elimu ya ufundi na wanaweza kurejea tena kusoma elimu ya Chuo Kikuu kwa mfumo huo wa elimu ya ufundi.
d)     Taifa litakuwa na vijana wengi wenye utaalamu wa fani mbalimbali, hivyo kuongezaka kwa ajira za kujiajiri kwa vijana hawa kwani wana elimu ya ufundi.
e)      Wimbi la ukosefu wa ajira pia utapungua kwa kiasi kikubwa kwani vijana wengi watakuwa wamejiajiri katika sekta mbalimbali
f)       Itakuwa ni rahisi sana kwa taasisi na wizara inayohusika na vijana kuwekeza kuboresha mitaji na shughuli za vijana kwani wengi watakuwa na utaalamu Fulani
g)      Itarahisisha kufika Tanzania ya Viwanda kwani tutakuwa na tabaka kubwa la vijana ambao wana utaalamu wa vitendo na ujuzi wa rasimali zote tulizonazo.
13)      Tuboreshe sana miundombinu ya elimu kama kuwa na waalimu wenye uwezo na wito, kuwa naa mazingira sanifu kwa walimu wetu, kumfanya mzazi awe mwalimu wa nidhamu ya mtoto pindi anaporejea nyumbani.
44)      Kila mmoja serikalini kuanzia Rais hadi Balozi wa nyumba kumi, amheshimu Mwalimu na aheshimu utaratibu uliowekwa na shule ilimradi tu hauvunji sheria za nchi. Nimeliongelea hili kutokana na hali niliyoona juzi na imekuwa ikiendelea kila siku kwa watumishi wa serikali. Hivi majuzi alitokea mkurugenzi wa halmashauri fulani, alimsimamisha kazi Mwalimu mkuu na Mwalimu wa taaluma kutokana na kosa la kuchangisha Sh.500 kwa kila mwanafunzi kwa ajili ya kuweka nembo ya shule kwenye sare zao. Mbaya zaidi lililoniumiza ni Mkurugenzi huyo kugonga kengele na kuwaita wanafunzi wote mstarini na kuwasisitiza kwamba hapana kuchangia chochote na kuwatajia kwamba wale walimu ameshawafukuza kazi. Hali hii inatengeza dhana ya watoto kuwadharau wanaowalea (Waalimu) na pia inawavunja moyo sana walimu wetu. Nakumbuka hata mama na baba wakigombana ndani ya nyumba watoto tukiingia wanatusalimia vyema na kuelekea chumbani kumaliza tofati zao ili watoto tusiige hiyo tabia lakini pia heshima iendelee kudumu.
Mama Ndalichako, nisikuchoshe kwa kuandika mengi ijapokuwa bado niko na mengi sana ya kunena. Naamini ipo siku tutakutana, nitakuelezea zaidi na kwa kina juu ya haya kwani naelewa toka enzi zile ukiwa Necta ulikuwa na nia ya dhati ya kufanya elimu yetu iwe na tija na iheshimiwe na kila mmoja ndani na nje ya nchi.
Mama Ndalichako, nikutakiwe maisha mema na yenye fanaka. Nikutakie utendaji kazi bora na Mungu aendelee kukupa hekima na busara ili uboreshe elimu yetu kwa maslahi ya watoto wetu na vizazi vijavyo.
Ni mimi,
Mkulima na mfugaji wa Kijiji cha Nadosoito

+255 756 688 090/+255 712 814 285

0 comments:

Post a Comment