Music

Monday, November 24, 2014

IFAHAMU UDSM PART 2


Ndugu mfuatiliaji wa kisa hiki, karibu ungana nami kwenye sehemu ya pili ya “unaifahamu Chuo Kikuu cha Dar es Salaam?” Kabla sijakudokeza wapi tuliishia wiki iliyopita, nisiwe mchoyo wa fadhila kukupeperushia zangu salamu zikukumbe popote ulipo. Bila hiyana nikupongeze pia kwa kunipa muda wako tena bure kabisa kwa kusoma mtiririko wa makala zangu kupitia kitovu cha fikra endelevu cha “Fukununu.blogspot.com”. Hii inanipa moyo wa kuzidi kuandika, kuanika na kuchimbua na kuibua mengi ambayo yapo nyuma ya pazia ama yanasikika kwa nadra sana kutokana na mfumo beberu na kandamizi ulioota mzizi ndani ya jamii yetu hii ya “adabu na utii kwa bwana mkuu” (Amani)

Najua wale wenzangu na mimi mtahoji sana kwanini amani iliyopo hapa nchini nimeifungia mabano na kuita ni adabu na utii kwa bwana mkuu. Mnaweza kufika mbali zaidi na kujiridhisha nafsini na mioyoni mwenu kwamba Ole anayafanya haya kutokana na mrengo na msimamo wake kisiasa. Sitowashangaa kwa hilo kwani imekuwa ada na jambo la kawaida kwenu kwa yeyote atakayewananga kwa lahaja za kweli bila kupepesa macho na kumung’unya maneno kuitwa “mpinzani”. Hivi kweli tunaweza kusema kuna amani ilihali kina “We-Lema, Tiba-Ibuka, Man-Swi, Chen-Ge, Kik-Ikweta, Pin-Ndao” na wale wengine wamechota bilioni 321 za Escrow huku walalahoi wakishinda kwa “suti” kuanzia asubuhi hadi asubuhi???? Kuna amani gani wakati bwana mkuu anatibiwa busha kwa Obama huku Matonya akijificha ndani kwa kudhuriwa na honi ya magari??? Kuna amani gani wakati mawazo yangu na wakulima wa Nadosoito yametupiliwa mbali kwenye mapendekezo ya katiba na kuchukua mawazo ya kikundi Fulani cha watu kilichojitengezea kanuni na sheria za kuwadanganya wananchi ili wapewe ridhaa ya kuongoza taifa???? Kuna amani gani kama watu wote wenye mawazo tofauti na wizi na ufisadi huchomolewa kucha na meno Mwabepande tena bila ya ganzi??? Kuna amani gani wakati kila mwaka bei ya bidhaa za chakula na gharama za maisha zinaongezeka kwa mwananchi wa kawaida huku tabaka la juu likizidi kujiimarisha kwa unyonyaji???? Kuna amani gani kama mtoto wa Ole Lengai kutoka En’donyo Kumur aliyefaulu kujiunga na masomo ya elimu ya juu anashindwa kusoma kwa kukosa mkopo huku mtoto wa “Afisa” aliyesoma ughaibuni akipata asilimia mia????? Kuna amani gani kama mke wangu anajifungulia chini na kitovu cha mtoto kukatwa kwa kipande cha jiwe kwa kukosekana kwa huduma za afya bora vijijini na miundombinu ya barabara???? Damn it!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!! Huu udanganyifu sasa uwe bayana kwa watu wa tabaka na rika zote wa jinsia mbalimbali pasipo kujali itikadi zetu za dini, kabila wala siasa. Narudia tena HATUNA AMANI BALI TUNA ADABU NA UTII KWA BWANA MKUU.
Baada ya kukuamsha hisia zako juu ya udokozi unaofanywa na hawa manyang’au wanaojificha kwenye mwamvuli wa chama Fulani cha siasa, sasa nikupeleke kwenye mada yetu kuntu ya wiki iliyopita hasa pale tulipoishia. Nilikuacha na ulumbi juu ya kufinywa kwa fikra na uhuru wa kutoa mawazo kwa vijana wasomi wa kitalu hiki. Sasa ungana nami kuendelea kurutubisha mawazo yako juu ya “the un-revealed story about UDSM”
Baada ya kufanikiwa kuzima malumbano ya mawazo miongoni mwa vijana wenye fikra sanifu na sadifu juu ya mhimili wa taifa letu, watu hawa ambao kwa majina hujulikana kama “maprofesa” wamezima pia uhuru wa kutoa mawazo kwa kutumia makala, vipeperushi na mabango. Awali chuo Kikuu cha Dar es Salaam kiliweza kuzalisha waandishi mahiri wa makala na wachambuzi wazuri wa mada mbalimbali kutokana na vijana wasomi wenye ukombozi wa fikra kujihusisha na uandishi wa makala na nakala mbalimbali na kubandika kwenye mbao za matangazo za UDSM. Tulikuwa na majarida kama Mlimani Leo, Mlimani Kesho, Fukununu na Wazo Pevu ambayo yalijikita kuchambua masuala mbalimbali ya kiuchumi, kielimu, kisiasa, kiutamaduni na kijamii yanayotokea ndani na nje ya nchi yetu ya Tanzania. Vijana waliokuwa wanajitutumua katika uandishi huu walipata moyo wa kuziendeleza karia hizi kutokana na kuwapata hadhira wengi ambao walitumia muda wao kusoma na kutoa mawazo yao juu ya mada zilizokuwa zikijadiliwa.
Baada ya kupitishwa kwa waraka wenye jina maarufu kama waraka wa Kawambwa ambao uliandaliwa mahususi kuzima mawazo pevu na hojaji zenye mrengo wa kutia mchanga kitumbua cha mabeberu wa nchi hii ambao ndio walioshikilia nafasi mbalimbali za kiutawala. Madubwana haya yaliona namna pekee ya kuzima mawazo kuntu kutoka kwa umajumui wa wasomi na wanazuoni wa elimu ya juu ni kuwadumaza kimawazo na kutowaruhusu kutawanya mawazo yao juu ya changamoto zinawakabili wananchi wa Tanzania.
Hali ya kutokea kwa dumuzi huyu ilianza kuonekana pale mkuu wa nchi Ndugu Kikwete alipozuru Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kampas ya Mlimani na kujikuta akipata tumbo joto baada ya kukutana na mabango yaliyoandikwa kisomi na yaliyobeba mada kuntu zenye kuelezea hali halisi ya maisha ya watanzania. Vilevile kila alipojitahidi kubwabwaja kama kawaida yake kuwadanganya watanzania, mkuu wa nchi alijikuta pia akikumbwa na zomea zomea kutoka kwa fikra zilizokamaa na zilizochoka na unyonyaji uliopo ndani ya nchi hii.
Kutokea kwa hali hii kuliamsha hisia za mabwanyenye wa nchi hii na kumshawishi kada mkuu na mshauri wa Baba Riz kwenye masuala ya kisiasa, Prof Mkandala kuwachukulia haraka sana ikiwa ni kuwafukuza masomo wanafunzi wote watakaohoji jambo lolote ndani ya chuo na vilevile “kifaranga” huyu akapewa rungu lenye mamlaka ya kuwanyima udahili kwenye vyuo vyote vya umma wanafunzi watakaokutwa na kadhia hii lakini zaidi pia ni kutopewa mikopo ya serikali tena hata kama watapata vyuo vya binafsi.
Hali ilivyo sasa ndani ya UDSM ni “mind your own business” kama ilivyo kwa shule za sekondari hasa zinazoongozwa na taasisi za dini. Jamii ile ya chuo Kikuu cha Dar es Salaam ambayo ilijulikana kama Think tank, kwa sasa tunaweza kuita ni Thin tank kwani kinachofanywa na wanaoitwa wasomi wa jamii hii ya mlimani ni “kupiga desa tu”…. Hata kuhoji kama chakula hakina chumvi vijana hawa wamebanwa na hawaruhusiwi kujielekeza kwenye hili kwani kwa tafasiri yao wanasema hali jiyo itaharibu amani ya chuo. Sasa swali, Je, kumfungia nyoka kwenye shimo na kuwasha moto juu yake, utakuwa umemaliza ukali wa huyo joka na utaweza kulala kwa amani? Tusije tuakawa tumezificha shida na kero za vijana wa elimu ya juu kwenye majani yenye urefu wa ndengu, huku karaha hizi zikiendelea kuota na kumea kila kuitwapo leo.
Ndugu msomaji, hali ilivyo sasa ndani ya UDSM ni hatari katika sekta mbalimbali za kiafya na kimawazo na kwa wale ambao mna mawazo kama yangu awali za kujiunga na UDSM kama kitovu cha mawazo na fikra endelevu, hicho kitu hakipo tena. Ni bora ukajiunga na vyuo vingine ambavyo unaweza kuendeleza karia yako nyingine mbali na masomo kwani ndani ya mlimani wanaoweza kufanya hivyo ni wale ngedere wa Hall 2 na 5.
@Comrade Ole

0 comments:

Post a Comment