Music

Tuesday, December 23, 2014

UDSM YAFUKUZA TENA, SAFARI HII NI VIONGOZI WA DARUSO



Image result for udsm
UDSM INAELEKEA WAPI???
Nawasalimu wote kwa salamu ya kikamaradi ambayo huamkiwa kwa fanani kusema; “Mbiu ya mnyonge” na hadhira kuitikia: “Ni kalamu”…!!!!!!!!!!!
Natumai wote hamjambo na mnaendelea vyema na maandalizi ya sikukuu za krisimasi na mwisho wa mwaka.

Kama mada inavyojitutumua kwa kichwa cha habari hapo juu, leo nimelenga kueleza hisia zangu kutokana na kile kinachoendelea ndani ya Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam ambayo naamini kinafanywa na utawala wa taasisi hiyo kubwa ya elimu chini ya “Prof” Mkandala.
Mwezi wa pili mwaka huu, niliandika makala ya kurasa nne niliyoipa jina la “Chuo Kikuu kimegeuga Choo Kikuu”. Makala hii ilijikita kutanabaisha hali ilivyo ndani ya Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam hasa katika uongozi na uhuru wa kuhoji, kutoa habari na maoni kwa vijana wasomi wa kitovu hiki cha elimu. Baada ya makala hiyo kutoka, wengi wanisifia kwa uthubutu wangu wa kuendelea na harakati za “kalamu” pamoja na maswaiba yaliyonipata. Wengine walinikebehi na kunikejeli kwa kusema nafanya hayo kisiasa na eneo hili si kwa ajili ya saisa bali ni kuongeza na kukuza maarifa ya vijana. Nami niliwajibu kwa kuwakumbusha maneno aliyowahi kuyatoa Mwalimu Nyerere akiwahutubiwa vijana ikulu mwaka 1964. Mwalimu alisema na namnukuu “…..Wajibu wenu ni kusoma. Lakini si kwa kusoma vitabu tu kwani mwaweza kusoma vitabu vingi bila kuwa na manufaa kwa jamii yenu. Hivyo msome huku mkisaidia jamii zenu kwani hapo ndipo tutakapoona manufaa ya elimu kwenu….”
Mwanzoni mwa mwezi huu niliendelea kutoa elimu kwa umma juu ya kile kilichopo ndani ya ya taasisi kubwa ya elimu hapa nchini yaani Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam. Makala hizi mbili nilizipa majina ya “Usiyoyajua kuhusu Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam part 1 & 2”. Makala hii ilijikita kuweka bayana hali halisi iliyopo ndani ya taasisi hii katika sekta muhimu za kiafya na malazi. Kama ilivyokuwa kwa makala ya awali, pia makala hizi mbili zilipokelewa kwa mitazamo tofauti na wadau mbalimbali kwa wengine kusifia na wengine kukosoa.
Hali imezidi kuwa mbaya sana kwa taasisi hii ya elimu kwani uhuru wa kutoa mawazo na uhuru wa serikali ya wanafunzi kujitawala umezidi kubanwa na kuendeshwa kwa maslahi ya watawala.
Hivi majuzi Rais wa serikali ya wanafunzi DARUSO, Bwana Nickson Filbert alikiuka katiba ya DARUSO kwa kufanya mambo mengi chini ya utaratibu wa kikatiba. Kwa kuwa wanafunzi wa kawaida hawaruhusiwi kuhoji masuala kama haya, wawakilishi wao yaani wabunge waliliona hili na kuishtaki Rais huyo kwenye chombo cha maamuzi ambayo hutumika kama mahakama hapo chuoni ambayo hujulikana kama DARUSO BOARD. Chombo hiki kipo kikatiba kwa mujibu wa katiba ya DARUSO na imeundwa na wenyeviti wa Collages, Schools na Institutes. Chombo hiki kina jukumu la kuhakikisha kwamba serikali inatawala kwa mujibu wa sheria na kwa kufuata katiba.
Kama ilivyo ada kwa shitaka lolote likifikishwa mahakamani, mshitakiwa hana budi kutoa utetezi wake kwa kujibu hoja. Vivyo hivyo kwa serikali ya DARUSO ilimtumia “Attorney General” wake ambaye anajulika kwa cheo cha Chief Protocal, kuiwakilisha serikali katika kutoa utetezi wa kesi inayoikabili. Chombo hiki kilisikiliza utetezi wa serikali na hatimaye kufikia maamuzi kwa kutoa hukumu kwamba serikali imekiuka katiba. Kosa la ukiukwaji wa katiba unafanya serikali kufika ukomo kwa Rais kuvuliwa madaraka yake na baraza la mawaziri kuvunjwa. Hii ni kwa mujibu wa katiba ya DARUSO.
Baada ya DARUSO BOARD kutoa uamuzi huu, inabidi bunge kukaa na kulipisha hilo ikiwa ni pamoja na kupata baraka za ofisi ya mshauri wa wanafunzi. Hili ni suala la kiutawala kwa serikali ya wanafunzi na ambao hauna mahusiano na utawala wa Chuo ikiwa tu umefanywa kwa kufuata kanuni, taratibu na sheria.
Pamoja na suala hili kufuata taratibu zote kisheria, utawala wa Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam umejiingiza kwenye sakata hili kwa KUWASIMAMISHA MASOMO kwa muda usiojulikana viongozi sita wa DARUSO BOARD na wabunge waliopeleka hoja hii kwenye chombo hiki cha uamuzi.
Nimesikitishwa sana na hali hii inayofanywa na Bwana Mkandala, Luoga na Mfinanga huku wakijua fika kwamba wanadumaza demokrasia ndani ya taasisi hii na kujenga kizazi cha vijana wasio na utashi na uwezo wa kujenga hoja na kuhoji hata masuala nyeti nay a msingi kwa mustakabali ya nchi yetu. Kutokana na hili nadiriki kusema Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam kimepoteza hadhi yake ya kujikosha kama Chuo Kikuu na ijulikane tu kama Chuo Cha Dar es Salaam kwani kuendelea kuweka neon “Kikuu” ni kudhalilisha taaluma zetu na kubariki kile kinachofanywa na wanafiki na wazandiki waliohodhi madaraka ndani ya taasisi hii.
Pia nitoe rai kwa wanafunzi wa Chuo hiki kufanya mambo makuu mawili kuonyesha kutokubaliana na hali hii inayoratibiwa na kufanywa na haya madubwanya na mafisadi wakubwa wa mawazo ya vijana.
Mosi, kutojihusisha kabisa na masuala yote yanayohusu upatikanaji wa serikali ya wanafunzi, yaani kutojitokeza kuchukua form za kugombea nafasi yoyote siku uchaguzi wa serikali ya wanafunzi utakapotangazwa. Hii ni kuonyesha kwamba hatuwezi kutafuta nafasi ambazo kiongozi hayupo huru kuwatumikia wanafunzi na kufanya kazi kwa mujibu wa katiba iliyopo bali kwa matakwa ya walowezi wa utawala.
Pili, Kutochangia kiasi cha Tsh. 10,000 ambayo inalipwa kila mwaka kama ada ya DARUSO kwani hakuna haja ya kutoa mchango kwa chombo ambacho hakifanyi kazi kwa uhuru na kwa kuwatumikia wanafunzi bali kwa kuwaabudu na kufuata taratibu za walowezi watawala hata kama ni kinyume na taratibu na yanakiuka katiba ya DARUSO. Kwa kufanya hivi tutakuwa tumezuia matumizi haya mabaya ya rasilimali za umma ambazo zinatumiwa na taasisi hii isiyokuwa na manufaa yoyote kwa walengwa.
Vijana wenzangu mliopo ndani ya taasisi hii, niwache na ujumbe huu kwa leo “….We have no alternative than to apply ourselves scientifically, physically and objectively to the problems facing our nation. We have to think about poverty, embezzlement of public resources, disobeys of rules and procedures and misuse of public resource that is taking place in every sector of our nation. From that context let us think on what best we can do for our nation to alleviate these….”
Asante sana
By Comrade Ole

0 comments:

Post a Comment